San’aa: UAE isubiri jibu chungu na la kuumiza

Mjumbe wa timu ya mazungumzo ya Serikali ya Uokovu wa Kitaifa ya Yemen amesema Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) unapaswa kusubiri jibu chungu na la kuumiza, na kwamba ni jambo la kawaida kujibu vitisho.

Abdul Malik al-Ajri amesema: “Utangulizi wa hatua ya Imarati kuingilia masuala ya ndani ya nchini Yemen ulianza pale Wamarekani walipopata yakini kwamba vita vya Maarib vinaelekea kumalizika na kwamba viko katika hatua muhimu na ya mwisho.”

Al-Ajri ameongeza kuwa, maadamu UAE imeingia vitani nchini Yemen italazimika kusubiri jibu la kuumiza, na kwamba kuendelea kwa vita hivyo kutaigharimu sana Imarati kuliko ilivyokadiriwa.

Mjumbe wa timu ya mazungumzo ya Serikali ya Uokoaji wa Kitaifa ya Yemen pia amesema kuwa vikosi vya jeshi la nchi hiiyo vinalenga tu wale wanaowalenga na kuwashambulia watu wa Yemen.

Hapo awali, kiongozi wa harakati ya Ansarullah ya Yemen, Abdul Malik al-Houthi alisema kwamba Wamarekani na utawala wa Kizayuni wa Israel wameilazimisha Imarati kuanzisha tena mashambulizi dhidi ya Yemen na kwamba Imarati ndiyo  itakayoshindwa katika mchezo huo.

Wakati huo huo Muhammad Al-Ghammari, mkuu wa vikosi vya majeshi la Serikali ya Uokovu wa Kitaifa ya Yemen, amesema ikiwa mashambulizi ya Imarati yataendelea, majeshi ya Yemeni yataanzisha mashambulizi mapya, makini na yenye nguvu zaidi ya uharibifu dhidi ya wavamizi hao.

Wiki iliyopita vikosi vya jeshi la Yemen vililenga miji mashuhuri ya Umoja wa Falme za Kiarabu ya Abu Dhabi na Dubai kwa makombora na ndege zisizo na rubani katika operesheni tatu za “Tufani ya Yemen-1”, “Tufani ya Yemen-2” na “Tufani ya Yemen -3”.

Previous Post
Next Post

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *