Katibu Mkuu wa Baraza la Kimataifa la Kukurubisha Pamoja Madhehebu za Kiislamu amesisitiza kuwa kulinda uthabiti, kujitawala na amani ya nchi za Kiislamu ni jukumu la Waislamu wote na akabainisha kwamba, ikiwa nchi isiyo ya Kiislamu itataka kuzivamia nchi za Kiislamu na kupora sehemu ya ardhi yake na utajiri wake, ni jukumu la kila mtu kusimama ili kuihami na kulinda ardhi hiyo.
Mkutano wa 15 wa Umoja wa Kiislamu umefanyika mjini London Uingereza kwa anuani ya “Kuelekea Maisha ya Kiutu na ya Hekima” kwa kuhudhuriwa na wanafikra na wasomi wenye vipawa wa Kiislamu.
Hujjatul Islam Hamid Shahriyari, Katibu Mkuu wa Baraza la Kimataifa la Kukurubisha Pamoja Madhehebu za Kiislamu amesema katika hotuba aliyotoa kwenye mkutano huo kwamba: kuzihami ardhi za Palestina ni lengo la pamoja la Waislamu wote.
Katibu Mkuu wa Baraza la Kimataifa la Kukurubisha Pamoja Madhehebu za Kiislamu ameendelea kueleza katika hotuba yake hiyo kuwa kuwahami na kuwaunga mkono watu wa Palestina, Iraq na Yemen na kulinda uthabiti na kujitawala kwa Syria, Lebanon na nchi zingine za eneo ni jukumu la nchi zote za Kiislamu na hasa maulamaa, wenye vipaji vya kisiasa, kidini na kiutamaduni pamoja na viongozi wa serikali na vijana wa vyuo vikuu.
Shahriyari ameongezea kwa kusema: kutokana na leo hii kuwepo nchi nyingi za Kiislamu kuna haja ya kuwepo mshikamano na ushirikiano kati ya nchi hizo ili kuweza kumshinda adui, ubeberu wa dunia na uzayuni.
Katibu Mkuu wa Baraza la Kimataifa la Kukurubisha Pamoja Madhehebu za Kiislamu ameeleza bayana kwamba “katika dini ya Uislamu hairuhusiwi makafiri kuwatawala na kuwahodhi Waislamu na hilo ni jambo lililokatazwa; na wala haifai Marekani au ajinabia yeyote yule awahodhi Waislamu; hii ndio mantiki na kaulimbiu yetu”.