Sisitizo la Nasrullah juu ya ulazima wa kuendelezwa Muqawama wa kukabiliana na adui Mzayuni

Sayyid Hassan Nasrullah, Katibu Mkuu wa Hizbullah ya Lebanon amesema, Muqawama ndio njia pekee ya kukabiliana na adui mzayuni. Nasrullah ameyasema hayo katika hotuba aliyotoa siku ya Jumamosi kwa mnasaba wa Arubaini ya Imam Hussein AS.

Hotuba ya siku ya Jumamosi ya Sayyid Hassan Nasrullah iliangazia mambo kadhaa, lakini moja ya nukta aliyoitilia mkazo ilikuwa ni jinai za utawala haramu wa Kizayuni wa Israel na kusisitiza kwamba, muqawama ndio njia pekee ya kukabiliana na jinai za adui huyo.
Nukta ya mwanzo aliyoiashiria Sayyid Hassan Nasrullah kuhusiana na suala hilo ilikuwa ni jinai ya Sabra na Shatila. Katika jinai hiyo iliyofanywa miaka 40 iliyopita, utawala wa Kizayuni uliwashambulia wakimbizi Wapalestina na wananchi wa Lebanon, ambapo mbali na Wapalestina 3,500, Walebanon 1,900 pia waliuawa shahidi katika jinia hiyo. Kwa maelezo ya Sayyid Hassan Nasrullah, jinai ya Sabra na Shatila ni jinai kubwa, ya kinyama na ya kutisha zaidi kuwahi kufanywa katika historia ya mapambano kati ya Waarabu na utawala wa Kizayuni; na kwamba Wazayuni na Walebanon waliohusika na jinai hiyo bado hawajaadhibiwa hadi sasa.

Kwa hivyo, moja ya sababu za kuendelezwa jinai za utawala wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina na hata Walebanon ni kwamba, kwa upande mmoja, utawala huo wa Kizayuni haukuadhibiwa wala kuchukuliwa hatua yoyote kwa kufanya jinai hiyo ya kutisha zaidi; na kwa upande mwingine, wahaini na wasaliti wa ndani ya Lebanon, nao pia si tu hawakuadhibiwa kwa kushirikiana na utawala huo, lakini wangali wako kwenye ulingo wa siasa za Lebanon wakiungwa mkono wa Wazayuni na waungaji mkono wao wa Magharibi. Na ndio kusema kuwa, maadamu hiyo ndio hali inayoendelea kutawala, jinai za utawala wa Kizayuni hazitakomeshwa, wala nchi kama Lebanon haitaweza kuwa na uthabiti wa kisiasa na kiusalama.

Nukta nyingine muhimu katika hotuba ya Sayyid Hassan Nasrullah ni kwamba, Marekani sio tu haiziungi mkono nchi za Lebanon na Palestina, bali kimsingi ni kwamba, dhamana na mahakikisho  inayotoa Washington ya kuziunga mkono nchi hizo na kukomesha jinai za Wazayuni si ya kuaminika wala kutegemewa. Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Hizbullah, “kukubali hakikisho na dhamana inayotoa Marekani ni sawa na kujipeleka machinjioni.” Akifafanua zaidi nukta hiyo, Sayyid Hassan Nasrullah amesema: “yeyote anayekubali dhamana na mahakikisho yanayotolewa na Marekani ni sawa na mtu anayekubali kuwapeleka wanaume, wanawake na watoto wake machinjioni kuchinjwa.”

Kimsingi ni kwamba, siasa na sera za Marekani ndio sababu kuu ya kuendelea jinai za Wazayuni, hususan dhidi ya Wapalestina. Muamala wa Karne, ambao ulibuniwa na kutekelezwa na serikali iliyopita ya Marekani ni miongoni mwa sera iliyoonyesha wazi kuwa lengo lake lilikuwa ni kukidhi maslahi ya utawala huo ghasibu na kukandamiza maslahi ya Wapalestina; na ukachochea zaidi kushadidishwa ukatili na jinai za utawala wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina. Baada ya kutekelezwa mpango huo wa kibaguzi wa Muamala wa Karne, utawala wa Kizayuni umeweza kuendeleza kwa wepesi zaidi na bila ya hofu yoyote mipango na njama zake dhidi ya Wapalestina.

Nukta ya kistratijia na kiini cha hotuba ya Sayyid Hassan Nasrullah kwa mnasaba wa Arubaini ya Imam Hussein AS ni kwamba, kuendelea jinai za utawala dhalimu wa Kizayuni wa Israel na sera za uungaji mkono wa Marekani kwa utawala huo zimethibitisha kuwa, muqawama ndio njia pekee ya kukabiliana na utawala huo unaoukalia mji wa Baitul Muqaddas (Jerusalem) kwa mabavu; na kwamba mazungumzo, sio tu hayatakuwa na manufaa yoyote kwa Wapalestina, lakini pia yatawafanya wapoteze nyenzo za kuwapa nguvu na uwezo, ukiwemo umoja na mshikamano wao. Kuhusiana na hilo, Sayyid Hassan Nasrullah amesisitiza kwa kusema “wananchi wa Palestina sasa wamefikia natija ya uhakika kwamba mazungumzo hayana faida yoyote na chaguo pekee lililopo mbele yao ni muqawama.”
Sasa hivi mwamko, ari na hamasa ya muqawama wa Wapalestina zimeenea katika maeneo yote ya Palestina inayokaliwa kwa mabavu na haiko kwa watu wa Ukanda wa Gaza pekee. Kwa mtazamo wa Sayyid  Hassan Nasrullah, kusambaa wimbi la muqawama miongoni mwa wananchi wote wa Palestina ni jambo ambalo adui hakulitarajia, na ni sawa na kusema kwamba, “adui alifanya makosa ya kimahesabu na sasa amenasa kwenye kinamasi”.
Previous Post
Next Post

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *