Viongozi wa Afrika Kusini wameikosoa serikali ya Marekani kwa kutoa tahadhari ya uwezekano wa kutokea shambulizi la kigaidi katika nchi hiyo ya kusini mwa Afrika.
Jana Ijumaa, Idara ya Taifa ya Operesheni za Pamoja na Intelijensia ya Afrika Kusini (Natjoints) iliwaonya wananchi wa nchi hiyo ya kusini mwa Afrika dhidi ya kusambaza taarifa za uwongo za kutokea mashambulizi ya kigaidi.
Luteni Kanali Robert Netshiunda, Msemaji wa idadi hiyo inayojumuisha Idara ya Usalama wa Taifa (SSA) na Jeshi la Polisi la Afrika Kusini (SAPS) amepuuzilia mbali indhari hiyo ya Marekani na kusisitiza kuwa, vyombo vya usalama nchini humo vimeweka mikakati ya kutosha ya kukabiliana na vitisho kwa usalama wa taifa.
Siku ya Alkhamisi, Rais Cyril Ramaphosa alikosoa tahadhari hiyo ya Marekani na kusema, “Inasikitisha kuona ubalozi wa Marekani unatoa tahadhari ya uwezekano wa kutokea hujuma ya kigaidi wikendi hapa nchini pasi na kuishauri au kufanya mazungumzo yoyote nasi.”
Ramaphosa amesisitiza kuwa: Tahadhari yoyote inapaswa kutolewa na serikali ya Afrika Kusini, lakini kwa bahati mbaya serikali nyingine imetoa tahadhari hiyo ili kuibua hofu miongoni mwa watu wetu.
Naye Zizi Kodwa, Waziri wa Usalama wa Ndani wa Afrika Kusini amesema wizara hiyo imebughudhiwa na hatua ya Ubalozi wa Marekani kutoa indhari bila kuwasiliana nayo na kuwasilisha ushahidi wa kuyapa nguvu madai yake.
Siku ya Jumatano, Ubalozi wa Marekani nchini Afrika Kusini ulitoa tahadhari hiyo na kudai kuwa, yumkini hujuma hiyo ya kigaidi ikatokea leo Jumamosi katika eneo la Sandton, viungani mwa jiji la Johannesburg.