Amnesty: Israel imefanya ‘jinai ya kivita’ kwa kumtimua mwanaharakati wa Kipalestina

Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limesema hatua ya Israel ya kumfukuza mwanaharakati wa kutetea haki za binadamu Salah Hammouri, Mfaransa mwenye asili ya Palestina, ni jinai ya kivita.

Diana Eltahawy, Naibu Mkurugenzi wa Amnesty International katika eneo la Mashariki ya Kati na Kaskazini mwa Afrika (MENA) amesema, kufukuzwa kwa Salah Hammouri kumeonesha kwa mara nyingine tena namna mamlaka za Israel zinavyokanyaga wazi sheria za kimataifa.

Aidha amesema hatua ya Wazayuni ya kumtimua mwanaharakati huyo wa kutetea haki za binadamu imeanika machoni pa ulimwengu sheria na sera za kibaguzi za Israel ambazo ndio msingi wa mfumo wa ubaguzi wa apartheid wa utawala huo.

Afisa huyo mwandamizi wa shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International ameeleza bayana kuwa, Israel imemtimua Hammouri ili kujaribu kuficha madhila na mateso aliyoyapitia mwanaharakati huyo kwa muda wa mwaka mzima.

Ameongeza kuwa, kutimuliwa kwake bila hata ya kufunguliwa mashitaka ni sehemu ya mwisho ya kampeni ya mamlaka za Israel ya kumuadhibu mwanaharakati huyo, kutokana na jitihada zake za kutetea haki za binadamu, na vile vile inaonesha mkakati wa Tel Aviv wa kutaka kupunguza idadi ya Wapalestina katika mji wa Quds (Jerusalem).

Kwa mujibu wa shirika la habari la WAFA, Salah Hammouri, wakili, mwanaharakati na mtafiti wa shirika lisilokuwa la kiserikali la Addameer linalojihusisha na masuala ya sheria na kutetea haki za wafungwa, alifukuzwa katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na utawala wa Kizayuni mnamo Disemba 18 na kupelekwa Ufaransa, baada ya kuzuiliwa kwa miezi tisa bila kufunguliwa mashitaka.

Previous Post
Next Post

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *