Iran na Afrika Kusini zimelaani vikali jinai za kinyama zinazoendelea kufanywa na utawala wa Kizayuni dhidi ya wananchi wasio na ulinzi wa Ukanda wa Ghaza huko Palestina.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Nasser Kana’ani amelaani jinai hizo na kuilaumu jamii ya kimataifa na mashirika yanayojigamba kutetea haki za binaadamu, kwa kukaa kimya mbele ya jinai hizo za Wazayuni.
Msemaji huyo wa Wizara ya Mambo ya Nje ya iran amesema, hii ni mifano ya wazi ya jinai dhidi ya binadamu na ukatili unaotokana na fikra za ubaguzi wa rangi na kizazi uliojikita ndani ya utawala wa Kizayuni wa Israel.
Kwa upande wake, Wizara ya Mambo ya Nje ya Afrika Kusini imetoa taarifa rasmi ya kulaani jinai za Israel huko Ghaza na kusema kuwa, jamii ya kimataifa ina wajibu wa kudhamini usalama wa raia wa Palestina kama zinavyosema sheria za kimataifa. Hivyo inapaswa kuchukua hatua za kweli za kuulazimisha utawala vamizi wa Kizayuni ukomeshe mashambulizi yake dhidi ya raia hususan wanawake na watoto wadogo wa Ukanda wa ghaza.
Wimbi la kulaaniwa Israel limeongezeka sana hivi sasa kutokana na ukatili wake wa kupitiliza mipaka inaoufanywa dhidi ya wakazi wa Ghaza ambao imewazingira kila upande kwa miaka mingi sasa.
Hivi sasa maeneo mbalimbali ya ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni yanashuhudia maandamano makubwa ya kulaani jinai hizo za utawala wa Kizayuni huko Ghaza.