Mataifa jirani ya Kenya na Somalia yameazimia kufungua mpaka kwa awamu, ndani ya siku 90 zijazo.
Akitoa tangazo hilo jana Waziri wa Mambo ya Ndani wa Kenya Kithure Kindiki alisema kuwam mpaka wa Mandera/Belet Hawo (Belethawa) utakuwa wa kwanza kufunguliwa katika muda wa siku 30 zijazo.
Sehemu hii ya mpaka inatoa kiingilio kutoka upande wa Kenya katika Kaunti ya Mandera.
“Katika awamu ya pili ambayo ni siku 60 kutoka sasa, tunafaa kuwa na uwezo wa kufungua mpaka wa pili Liboi-Harhar/Dhobley. Hii itatoa kiingilio kutoka kaunti ya Garisa,” alisema.
Aidha kwa mujibu wa Wzairi Kindiki, awamuu ya tatu ya mpaka itakayofunguliwa itakuwa Kiunga/Ras Kamboni huko Lamu.
Waziri Kindiki alithibitisha kuwa serikali ya Kenya itaendelea kushirikiana na Serikali ya Shirikisho la Somalia ili kuendeleza na kutekeleza mbinu na mikakati ya pamoja katika masuala ya kiuchumi na kupambana na ukosefu wa usalama katika mipaka ya nchi hizo mbili.
Kwa upande wake, Mohamed Ahmed Sheikh Ali Waziri wa Mambo ya Ndani wa Somalia alisema serikali ya Shirikisho imejitolea kukuza na kuimarisha ushirika na majirani zake ili kuimarisha usalama. Wawili hao pia waliazimia kuimarisha mawasiliano ya mipakani na upashanaji habari kati ya nchi hizo mbili.
Mipaka ya nchi mbili hizo ilifungwa mwaka 2011 katika kilele cha mashambulizi ya kundi la wanamgambo wa al Shabaab.