Israel kuwekewa vikwazo na Umoja wa Ulaya kutokana na jinai zake Rafah
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Ireland amesema kuwa, kwa mara ya kwanza Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni wa Umoja wa Ulaya wamejadili kwa kina uwezekano wa kuuwekea vikwazo utawala wa Kizayuni iwapo hautatekeleza amri ya Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) ya kusimamisha mashambulizi ya kijeshi dhidi ya Rafah.
Michael Martin Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Ireland amewaambia waandishi wa habari baada ya mkutano wa Baraza la Mahusiano ya Kigeni la Umoja wa Ulaya kwamba, kwa mara ya kwanza katika mkutano wa Umoja wa Ulaya, nilishuhudia kwa uwazi mjadala muhimu kuhusu vikwazo dhidi ya Israel.
Pamoja na hayo ameeleza kuwa: Hakuna maafikiano yaliyofikiwa katika suala hilo, lakini watu wanasisitiza kuwa iwapo Israel haitazingatia hukumu za Mahakama ya Kimataifa ya Haki, ni vyema kuchukuliwa hatua ya kuiwekea vikwazo Israel.
Ijumaa iliyopita, Mahakama ya Umoja wa Mataifa iliuamuru utawala wa Kizayuni wa Israel usitishe mara moja mashambulizi yake katika mji wa kusini mwa Gaza wa Rafah na kujiondoa katika eneo hilo, kufuatia kesi iliyowasilishwa na Afrika Kusini ikiishutumu Israel kwa kufanya mauaji ya kimbari, na kuielezea hali hiyo kuwa ni hatari kubwa kwa wakazi wa Palestina.
Mawakili wa Afrika Kusini walikuwa wameitaka mahakama ya ICJ yenye makao yake mjini The Hague kuchukua hatua za dharura, wakisema mashambulizi ya utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya Rafah lazima yakomeshwe ili kuhakikisha usalama wa maisha ya Wapalestina.