Milipuko miwili ya mabomu imeuwa raia wasiopungua tisa na kujeruhi wengine kadhaa katikati ya Somalia.
Abdullah Adam afisa usalama wa Somalia amesema kuwa watu wasiopungua 9 wameuawa na wengine 15 wamejeruhiwa katika milipuko miwili ya mabomu ya kutegwa ndani ya gari iliyotokea kwa wakati mmoja mapema leo Jumatano katika mji wa Mahas kwenye mkoa wa Hiran katikati mwa Somalia.
Maafisa usalama katika mji huo wameeleza kuwa, magaidi wameushambulia mji wa Mahas mapema leo asubuhi kwa kutumia magari yaliyosheheni mada za milipuko. Magaidi hao walilenga eneo la raia ambapo watu 9 wamethibitishwa kupoteza maisha, wote wakiwa ni raia wa kawaida.”
Watu walioshuhudia hujuma hiyo wameeleza kuwa milipuko hiyo ilitokea mkabala wa mgawaha mmoja karibu na ofisi ya mkuu wa wilaya katika mji wa Mahas ambapo wanawake na watoto ni kati ya wahanga tisa waliopoteza maisha.
Hujuma hiyo ya leo katikati mwa Somalia inadaiwa kufanywa na kundi la kigaidi la al Shabaab ambalo limekuwa likifanya mashambulizi dhidi ya serikali ya Mogadishu na kuwauwa watu tangu mwaka 2006.
Mashambulizi hayo pacha ya milipuko ya mabomu yametokea mapema leo katikati mwa Somalia huku vikosi vya ulinzi vya nchi hiyo na kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Afrika (ATMIS) vikizidisha oparesheni za kijeshi dhidi ya kundi la kigaidi la al Shabaab lenye mfungamano na mtandao wa al Qaida.