FARAAN: NAIBU Rais Willam Ruto Jumamosi ameidhinishwa kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022.
Hii ni mara ya kwanza kwa mwanasiasa huyo ambaye alichaguliwa kwa mara ya kwanza kuwa Mbunge wa Eldoret Kaskazini mnamo 1997, kujitosa rasmi katika kinyang’anyiro cha urais nchini.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Wafula Chebukati amesema Dkt Ruto alitimiza mahitaji yote kuidhinishwa kama mgombea urais.
Mgombea mwenza wake Rigathi Gachagua pia ameidhinishwa baada ya stakabadhi zote kubainika kuwa sawa.
“Ombi la William Ruto na mgombea mwenza wake la kutaka kushiriki katika uchaguzi wa urais Agosti 9, 2022 limekubaliwa,” akasema Bw Chebukati huku viongozi wa Kenya Kwanza, na wafuasi wa Dkt Ruto, wakishangilia.
Dkt Ruto alielezea Imani yake kwa IEBC katika jitihada zao za kuhakikisha kuwa uchaguzi mkuu ujao utaendeshwa kwa njia huru na haki na ambayo matokeo yake yataaminika.
“Ni furaha yangu kupokea cheti ambacho kitaniruhusu mimi na naibu wangu kushiriki katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022. Bw Mwenyekiti, tumejitolea kudumisha kanuni ya nidhamu ambayo tumetia saini. Tuna imani kuwa umehitimu kazi hii na tutashirikiana nawe kwa dhati,” Dkt Ruto akasema.