Umoja wa Mataifa unasema mwaka 2022 unasalia kuwa mwaka mbaya zaidi kwa Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi tangu 2005, huku katika kipindi cha mwezi mmoja Wapalestina 19 wakiuawa shahidi katika mashambulizi ya wanajeshi wa utawala haramu wa Israel katika maeneo yanayokaliwa kwa mabavu na utawala huo.
Ripoti ya kila wiki ya Ulinzi wa Raia iliyochapishwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA) huko Palestina, imesema wanajeshi wa Israel wamewaua kwa risasi Wapalestina 19, wakiwemo watoto watatu, katika matukio tofauti katika maeneo yanayokaliwa kwa mabavu kati ya Novemba 22 na Disemba 11.
Mvulana wa Kipalestina mwenye umri wa miaka 16 aliuawa Novemba 22 nje kidogo ya mji unaokaliwa kwa mabavu wa Ukingo wa Magharibi wa Nablus, ripoti hiyo imesema, na kuongeza kuwa mtoto mwingine mwenye umri wa miaka 16 aliuawa karibu na mji wa Aboud, kaskazini magharibi mwa Ramallah, tarehe 8 Desemba. Msichana mwenye umri wa miaka 15 pia aliuawa katika mji wa kaskazini wa Jenin katika Ukingo wa Magharibi mnamo Desemba 11, kulingana na ripoti ya OCHA.
Mnamo Novemba 29, ndugu wawili wa Kipalestina waliuawa kwa risasi za moto katika kijiji cha Kafr Ein karibu na Ramallah na mwanamume wa Palestina aliuawa na afisa wa polisi wa mpaka wa Israel katika mji wa Huwwara, kusini mwa Nablus mnamo Desemba 2. Aidha Mpalestina mwingine pia alifariki dunia kutokana na majeraha aliyopata hapo awali.
Mbali na mauaji hayo, vikosi vya Israel vimeziba njia kuu za kuingilia katika vijiji kadhaa katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan, na hivyo kuvuruga maisha ya maelfu ya Wapalestina, ripoti hiyo imesema.
Wakati huo huo, wataalamu wa Umoja wa Mataifa wamelaani ghasia za walowezi wa Kizayuni na matumizi ya nguvu kupita kiasi yanayofanywa na jeshi la Israel katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari, wataalamu hao wa Umoja wa Mataifa wamekashifu “kukithiri kwa ghasia za walowezi wa Kizayuni na matumizi ya nguvu kupita kiasi yanayofanywa na wanajeshi wa Israel dhidi ya Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu mwaka huu, ambayo yameufanya mwaka 2022 kuwa mbaya zaidi katika eneo hilo la ardhi ya Palestina inayokaliwa kwa mabavu tokea Umoja wa Mataifa ulipoanza kuweka kumbukumbu za vifo mwaka 2005.”