Duru za Kizayuni zimedai kuwa, Harakati ya Jihad al Islami ya Palestina imeweka tayari kwa ajili ya kufyatuliwa makombora zaidi 3000 baada ya kiongozi wake mmoja kukamatwa katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Mapema Jumanne asubuhi, wanajeshi wa utawala wa Kizayuni waliivamia kambi ya wakimbizi ya Jenin na kumuua shahidi Mpalestina mmoja na kumteka nyara Bassam al Saadi, mmoja wa makamanda wa ngazi za juu wa harakati ya Kiislamu ya Jihad al Islami na kumpeleka kusikojulikana.
Baada ya tukio hilo, duru za Kizayuni zimedai kuwa, katika kipindi cha siku tatu zilizopita, harakati ya Jihad al Islami imeweza kutoa chini ya ardhi na kupandisha juu makombora yake yasiyopungua 3,200 na kuyaweka tayari kwa ajili ya kufyatuliwa.
Mapema Jumanne asubuhi, harakati ya mapambano ya Kiislamu ya Jihad al Islami ya Palestina ilitoa onyo kali kwa Wazayuni na kuiambia Israel kuwa, iwapo kiongozi wake huyo, Sheikh Bassam al Saadi. atapata madhara yoyote, basi ijiandae kwa majibu makali.
Wakati huo huo walowezi wa Kizayuni wanaoishi kwenye vitongoji vilivyoko karibu na Ukanda wa Ghaza wamesema kuwa, wanafikiria kuhama kabisa katika ardhi za Palestina baada ya harakati ya Jihad al Islami kutoa onyo kali kwa utawala wa Kizayuni.
Ripoti hiyo imesema kuwa, walowezi wengi wa Kizayuni wanaofanya kazi katika mashamba ya kilimo wanaogopa kuukaribia mpaka wa Ukanda wa Ghaza na wamevunjwa moyo na jeshi la Israel kwa kushindwa kuwalinda mbele ya makombora ya wanamapambano wa Palestina.